Huku ikiwa nimesalia chini ya wiki moja tu kabla ya msimu wa 2014/2015
kuanza, mambo yanaendelea kutokota kuhusiana na suala la usalama wa
viwanjani. Katika mji wa kaskazini wa Bremen, maafisa wametangaza kuwa
kampuni inayohusika na ligi kuu ya Ujerumani, DFL – Deutsche Fußball
Liga GmbH, itaanza kuwalipa polisi ambao watatumika katika mechi za
ligi.
Na sasa jimbo la North Rhine Westphalia NRW limetangaza kuwa polisi wa
eneo hilo watapunguzwa katika viwanja vya michezo.
Au katika baadhi ya
matukio hawatahitajika kabisa katika mechi za Bundesliga za eneo hilo
kuanzia msimu huu. Jimbohilo ni mojawapo ya maeneo ya vilabu vingi vya
Bundesliga: ni nyumbani kwa timu sita za Bundesliga – Dortmund, Schalke,
Cologne, Leverkusen, Borussia Moenchengladbach na Paderborn.
Kwa mujibu wa mipango iliyotangazwa waziri wa mambo ya ndani Ralf Jäger,
polisi watawekwa “katika maeneo yaliyofichika na pia watatumika kwa
kiwango kidogo sana kuyasindikiza makundi ya mashabiki”.
Hii ni kutokana na gharama kubwa zinazotolewa kwa polisi wanaotoa ulinzi
katika mechi za Bundesliga. Sasa mashabiki wanaombwa kuwajibika
wenyewe. Kama hilo litafanikiwa au la, tutaweza kuona wakati mechi za
ligi zitakapoanza wiki ijayo..
Hata hivyo hatua hiyo ya Kupunguzwa polisi katika mechi za Bundelsiga
haichukuliwi katika miji yote ya Ujerumani. Berlin kwa mfano
imethibitisha kuwa haitajihusisha na mpango huo wa majaribio kwa wakati
huu.
Katika ligi nyingine kuu za Ulaya, kwa miaka mingi vilabu hutakiwa
kugharamia malipo ya polisi wanaotoa ulinzi. Vilabu vya Ufaransa kwa
mfano, hulipa sehemu ya gharama za malipo ya polisi wakati wa siku ya
mchuano. Katika ligi ya Uhispania Primera Division na Premier League ya
England, serikali huwalipa polisi wanaoweka ulinzi nje ya wiwanja pekee.
Nchini Uhispania, vilabu hasa hutumia kampuni za kibinafsi za usalama,
ndani ya viwanja ili kuwathibiti mashabiki. Nchini England, ni jukumu la
vilabu kuhakikisha usalama wa ndani ya viwanja vyao.
No comments:
Post a Comment