Maandalizi mazuri, uwekezaji mkubwa wa miundombinu na
utaalam na usajili mzuri yameipatia Azam FC ushindi mnono kwa kuifunga
Mtibwa Sugar 4-1 katika mchezo wa ligi kuu ya Vodacom uliochezwa kwenye
Uwanja wa Manungu, Turiani mkoani Morogoro.
Ushindi huo wa ugenini umeiongezea Azam FC pointi tatu na kufikisha
jumla ya pointi 33 ikiwa sawa na Yanga wakitofautiana kwa magoli, na
Simba kuwa ya tatu ikiwa na pointi 27.
Katika mchezo huo ujio mpya wa mchezaji Kipre Tchetche pamoja na
kandanda safi lililochezwa na Azam FC limeipatia ushindi timu hiyo na
kuongeza rekodi ya kuifunga timu Mtibwa kwa mara ya nne ikiwa katika
uwanja wa nyumbani kwao Manungu.
Azam FC walianza mchezo huo wakijiamini na mapema katika dakika ya 14
mchezaji Jockins Atudo aliipatia Azam FC goli la kwanza akimalizia
krosi iliyopigwa na Abdi Kassim ‘Babi’.
Dakika ya 21 Vincent Barnabas akaisawazishia Mtibwa Sugar kwa mpira
wa kichwa baada ya kuteleza kwa kipa Mwadini Ally wakati akitaka kudaka
mpira aliorudishiwa kwa kichwa na beki Jockins Atudo, timu zikaenda
mapumziko zikiwa sare ya 1-1.
Kipindi cha pili kilikuwa cha Azam FC, walipata goli la pili dakika
47 lililofungwa na mshambuliaji Brian Umony aliyecheza vizuri na
Humphrey Mieno na kuwapoteza mabeki wa Mtibwa na kuandika goli hilo
ambalo lilibadili matokeo yakawa 2-1.
Azam FC walifanya mabadiliko dk 45 alitoka Himid Mao akaingia Ibrahim
Mwaipopo alieyefanya kazi nzuri kipindi cha kwanza, dk 60 Abdi Kassim
alipumzishwa baada ya kuitendea haki safu yake ya ushambiliaj nafasi
yake ikachukuliwa na Tchetche Kipre na dk 75 alitoka Brian Umony
aliyefunga goli la pili akaingia kiungo Jabir Aziz.
Mabadiliko hayo yaliimarisha kikosi cha Azam FC na kuzidi kuitesa
Mtibwa Sugar ambao walionekana kupata tabu, dk 88 Kipre Tchetche
aliipatia Azam FC goli la tatu kwa shuti akimalizia mpira aliotengewa na
Humphrey Mieno na kupeleka matokeo kuwa 3-1.
Mshambuliaji huyo (Kipre) kutoka Ivory Coast alitumia vizuri dakika
za nyongeza kwa kuipatia Azam FC goli la nne na kuhitimisha kalamu ya
magoli baada ya kuunganisha vizuri mpira uliopigwa na nahodha Salum
Abubakar ‘Sure Boy’ na kumaliza mchezo Azam FC ikiondoka na ushindi wa
4-1 dhidi ya wenyeji wao Mtibwa Sugar.
Azam FC ilianza safari ya kurejea jijini Dar es Salaam mara baada ya
mchezo huo kwa ajili ya kuanza maandalizi kwa ajili ya mchezo wao wa
kwanza wa kimataifa katika mashindano ya Kombe la Shirikisho Afrika
dhidi ya Al Nasri Juba ya Sudan Kusini utakaochezwa wiki ijayo jijini
Dar es Salaam.
Kikosi cha Azam FC kilichofanya mauaji kiliundwa na Mwadini Ally,
Himid Mao/Ibrahim Mwaipopo 45’, Malika Ndeule, Jockins Atudo, David
Mwantika, Michael Bolou, Brian Umony/Jabir Aziz 75’, Salum Abubakar
‘Sure Boy’ (cpt), Abdi Kassim ‘Babi’/Tchetche Kipre 60’ Humprey Mieno na
Khamis Mcha
No comments:
Post a Comment