Bingwa Mtetezi wa mbio za New York Marathon Geoffrey
Mutai alitoka nyuma na kuthibitisha udedea wake katika barabara za mji
huo wa Marekani alipokata utepe akitumia muda wa saa moja na sekunde
hamsini.
Muingereza Mo Farah, hata hivyo, ndiye
aliyewaduwaza mashabiki wake nchini Marekani alipokunguwaa na kuanguka
baada ya takriban kilomita tisa na kisha akajifua na kurejea kwa
kishindombio zikikaribia kukamilika .
Bingwa huyo wa mbio za mita elfu
tano na mita elfu kumi za olimpiki alimaliza katika nafasi ya pili
sekunde 18 pekee nyuma ya Mkenya mshikilizi wa muda bora katika mbio za
marathon duniani.
Farah alishikwa na kisunzi punde baada ya kukamilisha mbio hizo na alilazimika kubebwa kwa machela.

Mo Farah azirahi baada ya kukamilisha mbio za New York
Muingereza huyo baadaye alisema alikuwa sawa na
kuwa ataendelea na mazoezi yake kabla ya kushiriki mbio zake za kwanza
za marathon katika mashindano ya London Marathon zitakazoandaliwa mwezi
ujao.
Mkenya mwengine Stephen Sambu alimaliza katika nafasi ya tatu sekunde moja pekee nyuma ya Mo .
Ilikuwa siku njema kwa wakenya kwani Sally
Kipyego vilevile kutoka Kenya alitwaa ubingwa wa kitengo cha wanawake
akisajili muda wa saa moja dakika 8 na sekunde 31.
Muda huo ndio wa kasi zaidi katika kitengo hicho cha wanawake.
Bizunesh Deba, kutoka Ethiopia alimaliza wapili huku Mmarekani Molly Huddle akikamilisha orodha ya tatu bora.
Wanariadha 20,000 walistahimili kiwango cha nyuzijoto zaidi ya 30 na kushiriki mbio hizo za kilometer 21 .
No comments:
Post a Comment