COASTAL
Union, leo imekubali kipigo cha bao 1-0 dhidi ya wenyeji wao nchini Oman, Fanja
SC inayoshika nafasi ya tano katika ligi kuu ya nchi hiyo mchezo uliopigwa uwanja wa Fanja
Club.
Bao la
Fanja, liliwekwa wavuni dakika ya 25 na Mohammed Maashari, baada ya
kupokea pasi ya kichwa kutoka kwa mshambuliaji hatari wa Fanja raia wa Senegal,
ambae alikuwa mfungaji bora msimu uliopita, Ely Cisse.
Mohammed
alipokea pasi ya Cisse kabla ya kupata nafasi ya kukutana uso kwa uso na mlinda mlango wa Wagosi wa
Kaya Shaaban Kado na kuchagua upende wa kushoto wa Kado kuutumbukiza mpira wavuni.
Baada ya
hapo Fanja, waliongeza kasi wakiamini wataongeza bao la pili lakini vijana wa
Coastal Union walikuwa makini kuhakikisha hawaondoki na kapu la mabao katika mchezo huo.
Mara nyingi
Danny Lyanga na Kenneth Masumbuko, waliingia ndani wakisaidiana na mtu mzima Haruna
Moshi ‘Boban’, lakini mpaka mwamuzi wa mchezo huo Majid Salim anapuliza kipyenga
kuashiria mapumziko bado ubao uliendelea kusomeka 1-0.
Kipindi cha
pili Fanja walifanya mabadiliko ya mlinda mlango na wachezaji wengine watatu
lakini Coastal Union iliendelea na kikosi chake kilichoanza awali.
Mchezo ulianza
kwa kasi huku Fanja wakionekana wamechoka, lakini Wagosi wa Kaya wakaendelea
kukosa mabao ya wazi yaliyowaumiza mashabiki wachache waliokuwa nje
kuwashabikia.
Ilipofika dakika
ya 70 Othman Tamim, alichonga kona upande wa kulia mwa uwanja ambayo ilipita
usoni mwa wachezaji wawili wa Coastal Union Masumbuki na Danny, bila kufanya
chochote ingawa Nahoda wa Wagosi Juma Nyoso alimbana golikipa wa Fanja ili
kuwapa nafasi washambuliaje wake watumbukize wavuni lakini haikuwa hivyo na
kukosa bao la wazi ambalo lingekuwa la kusawazisha.
Ilipofika dakika
kumi kabla ya mchezo kuisha kocha Yusuf Chipo alifanya mabadiliko kwa kumtoa
Atupele Green, akamuingiza Mohammed Miraji, ambae dakika moja baada ya kuingia
alimshinda mbio mlinzi wa Fanja akakabiliana uso kwa uso na golikipa wa klabu
hiyo lakini akapaisha.
Dakika tano
za mwisho Coastal Union walimiliki mpira na kuwachezea Fanja nusu uwanja hali
iliyoonyesha matokeo yangeweza kusomeka 1-1 muda wowote, lakini filimbi ya
mwisho iliwanyongonyeza wachezaji wa Coastal union.
Kwa matokeo
hayo Coastal Union ambao wapo Muscat Oman, kwa ziara ya wiki mbili wamepoteza
mchezo mmoja katika minne ambayo wamepanga kucheza wakiwa hapa.
Michezo miwili
ya awali walifanikiwa kuibuka kifua mbele kwa kuwachapa mabao 2-0, Al Mussannah
Club, inayoshika nafasi ya saba katika ligi ya Oman. Vilevile wakawachapa 2-0
klabu ya Oman Ckub inayosiriki ligi daraja la kwanza nchini hapa.
Mechi ya nne
itakayochezwa na Coastal Union ni dhidi ya Seeb Club, inayoshika nafasi ya nne
katika ligi ya hapa. Ingawa zipo taarifa kuwa kutakuwepo mechi ya tano, lakini
mpaka sasa wenyeji wetu hawajatoa maelezo ya moja kwa moja kuwa itakuwepo ama
la.
Baada ya
mechi kocha wa Fanja SC, Hisham Gidran alimwambia mwandishi wetu kuwa
ameshangaa kuona Coastal Union inacheza soka la kueleweka namna hiyo mbali ya
kushika nafasi za chini katika ligi ya Tanzania.
“Inaonekana
ligi ya Tanzania imekuwa ngumu, maana mmecheza soka safi sikutegemea, maana
nimeona katika msimamo wa ligi mpo nafasi za chini, naamini mtafanya vizuri
ikiwa mtacheza namna hii,” alisema.
Nae kocha wa
Coastal Union, Yusuf Chipo alipokuwa akishuka kwenye gari kuelekea hotelini
alisema hiyo gemu ilikuwa nzuri na ana cha kusema Zaidi ya hicho.
Shaaban
Kado, Hamadi Juma, Othman Tamim, Juma Nyoso, Marcus Ndeheli, Jerry Santo, Razakh
Khalfan, Kenneth Masumbuko, Danny Lyanga, Haruna Moshi, na Atupele Green. Baadae
alitolewa Atupele akaingia Mohammed Miraji.
No comments:
Post a Comment