KWA MAWASILIANO ZAIDI TUMIA BARUA PEPE rockersports212@yahoo.com AU TUPIGIE KUPITIA NAMBARI 0767166607 AU 0717166607. KARIBU SANA. 66666666607 AU 0717166607

Tuesday, January 8, 2013

YANGA YAGONGWA NA WAARABU WA ULAYA 2-1.(www.youngafricans.co.tz)

Wachezaji wa Young Africans wakisalimiana na wachezaji wa Denizlispor kabla ya kuanza kwa mchezo leo jioni.
Kikosi cha Young Africans kilichoanza dhidi ya Denizlispor fc katika mchezo wa kirafiki uliofanyika leo katika viwanja vya Selen Football - Kalemya Complex.
  Young Africans imepoteza mchezo wake wa kirafiki dhidi ya timu ya timu ya Denizlispor ya Uturuki kwa mabao 2-1 katika mchezo wa kirafiki uliofanyika katika viwanja wa Selen football - Kamelya Complex pembezoni kidogo ya mji wa Antalya.

Young Africans iliuanza mchezo kwa kasi kwa lengo la kusaka bao la mapema zaidi lakini umaliziaji wa washambuliaji  Saimon Msuva na Jerson Tegete katika dakika za 7, 15 na 24 uliikosesha mabao ya mapema.

Young Africans ndio iliyokuwa ya kwanza kupata bao kunako dakika ya 35, mfungaji akiwa ni Jerson Tegete akimalizia pasi safi iliyopigwa na Saimon Msuva kufuatia kugongeana vizuri na kiungo Haruna Niyonzima na Athuman Idd 'Chuji'.

Young Africans iliendelea kutawala mchezo kwa kipindi chote cha kwanza na hadi timu zinakwenda mapumziko Young Africans ilikuwa mbele kwa bao 1-0.

Kipindi cha pili Denizlispor ilifanya mabadiliko ya kikosi chake kuanzai mlinda mlango mpaka washambuliaji wake, lakini mabadiliko hayo bado hayakuweza kuisadia kwani umakini wa walinzi Kabange Twite, Nadir Haroub 'Cannavaro, Kelvin Yondani na Juma Abdul ulikuwa kikwazo kwao kumfikia mlinda mlango Ally Mustafa 'Barthez'.

Dakika ya 78 Denizlispor ilijipatia bao lake la kwanza baada ya mfungaji kupiga shuti lililokwenda moja kwa moja wavuni  ili hali walinzi wa Young Africans na mlinda mlango Ally Mustafa 'Barthez' wakisubiri kusikia filimbi ya mamuzi kwani mfungaji kabla ya kufunga alikuwa ameunawa mpira ndani ya eneo la hatari.

Huku mchezo ukiwa katika dakika za mwisho kabla ya kumalizika, mwamuzi wa mchezo ambaye hakuonekana kuwa makini aliwapatia wenyeji Denizlispor penati dakika ya 88, penati ambayo ilileta utata kutokana na mwamuzi kupishana maelekezo na mshika kibendera aliyekuwa ameonyesha kuwa mshambuliaji wa Denizlispor alikuwa amemfanyia madhambi nahodha Nadir Haroub, Denizlispor walipiga penati hiyo na kujihesabia bao la pili na la ushindi.
 Mpaka mwisho wa mchezo Young Africans 1- 2 Denizlispor FC.

No comments:

Post a Comment