MWALIMU Mwagane Yeya ‘Morgan’ leo ameondoka na mpira baada ya kufunga magoli matatu ya Mbeya City baada ya kwenda sare ya 3-3 na Azam FC kwenye uwanja wa Azam Complex huko Chamazi.
Mpaka mapumziko, timu hizo zilikuwa zimekwishafungana bao 1-1, Azam wakitangulia kupata bao kupitia kwa Humphrey Mieno dakika ya 13.
Kipindi cha pili, Mbeya City walitangulia kupata bao dakika ya 52 Mwagane Yeya tena akiunganisha kwa kichwa krosi ya Steven Mazanda, lakini John Bocco ‘Adebayor’ akaisawazishia Azam dakika ya 60 akiunganisha krosi ya Kipre Tchetche.
Mwagane tena akaifungia Mbeya City kwa shuti kali dakika ya 73 baada ya pasi ya Mazanda, lakini Khamis Mcha ‘Vialli’ aliyetokea benchi aliisawazishia Azam dakika ya 83, dakika tatu tu tangu aingie kuchukua nafasi ya Farid Mussa.
Katika uwanja wa taifa Yanga SC imepanda kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kufuatia ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya JKT Oljoro ya Arusha.
Mabao ya Yanga yamefungwa na Simon Msuva, Mrisho Ngassa na Jerry Tegete.
Kwa matokeo hayo, Yanga inamaliza mzunguko wa kwanza ikiwa na pointi 28 na kupaa kileleni, wakati Azam inashuka nafasi ya pili kwa pointi zake 27 sawa na Mbeya City, lakini inabebwa kwa wastani mzuri wa mabao ya kufunga na kufungwa.
Azam; Mwadini Ally, Erasto Nyoni, Waziri Salum, Said Mourad, Aggrey Morris, Kipre Balou, Salum Abubakar, Kipre Tchetche, John Bocco/Joseph Kimwaga 72, Humphrey Mieno na Farid Mussa/Khamis Mcha dk80.
Mbeya City; David Burhan, John Kabanda, Hassan Mwasapili, Deogratius Julius, Yussuf Abdallah, Anthony Matogolo, Mwagane Yeya, Steven Mazanda/Alex Sethi dk90, Paul Nonga/Francis Castor, Deus Kaseke na Richard Peter/Peter Mapunda dk46.

No comments:
Post a Comment