Matumaini ya kufanya vyema katika michuano ya kombe la kandanda la dunia
kwa timu ya taifa ya Ujerumani sio tu yapo kwa mashabiki wa soka wa
nchi hiyo bali hata kwa wadau wengine.
Rais wa chama cha soka cha Ujerumani Wolfagang Niersbach anakiri
kufurahishwa kwa kuanza vizuri kwa miamba hiyo ambayo iliichara Ureno
goli nne kwa bila kisha ikaenda sare ya goli mbili kwa mbili dhidi ya
Ghana.
Niersbach anasema anahisia sawa na mashabiki waliojitokeza mitaani
kushangilia ushindi dhidi ya Ureno kwani hakutarajia kuanza vizuri kiasi
kile katika michuano ya kombe la dunia tena dhidi ya timu inayoshika
nafasi ya tatu katika orodha ya viwango vya ubora ya shirikisho la
kandanda duniani FIFA.
"Ilikuwa ni kidogo kama mchezo dhidi ya Yugoslavia katika fainali za
mwaka 1990 mjini Milan, hivi karibuni nimempigia Franz Backenbauer nae
anafikiria hivyo hivyo" alisema Niersbach.
Niersbach anaongeza na kusema kuna vitu vinavyofanana na wakati ule
kwasababu Ujerumani ilikabiliana na timu imara na nafasi ya kila timu
kushinda ilikuwa ni 50/50 hivyo wengi hawakujua timu yao itachezaje.
Rais huyo wa shirikisho la soka la Ujerumani anasema hakuna shaka kwamba
uwezo na ari uliooneshwa na timu hiyo utaisaidia kufika mbali katika
mashindano hayo.
Kuhusiana na msisimko wa michuano ya kombe la dunia mwaka huu nchini
Brazil, Niersbach anasema alipata bahati ya kuwepo katika jiji la Sao
Paulo mapema wakati michuano hiyo ilipoanza na anakiri kuwa kulikuwa
hakuna ishara ya vitu ambavyo vinaashirikia mji huo utakuwa mwenyeji wa
fainali za kombe la dunia kama ilivyokuwa katika fainali za mwaka 2006
ambazo Ujerumani iliandaa, lakini Niersbach anasema ndani ya viwanja
kuna msisismko wa kutosha ambao unafanya fainali za mwaka huu kuwa na
mvuto wa aina yake.
No comments:
Post a Comment