Kikosi cha Nigeria katika kombe la dunia kimesusia
kikao cha mazoezi kama ilivyopangwa kwa sababu ya kukosa kulipwa fedha
zao za ziada.
Kitengo cha michezo cha BBC kimeelezwa kuwa
wachezaji hao wanaamini kuwa wamelipwa kiasi cha dola 15,000 (pauni
8,800), chini ya pesa wanazopaswa kulipwa baada ya kufika katika mkondo
wa pili wa kombe la dunia, huko Brazil.
Wachezaji hao wamesusia mazoezi
katika uwanja wa Campinas na baadaye maafisa wakadai kwamba mazoezi hayo
yalikuwa yametupiliwa mbali.
Nigeria inachuana na Ufaransa katika mechi ya
muondowano siku ya Jumatatu baada ya kuchukua nafasi ya pili katika
kundi lao la F.
Shirika la habari la BBC michezo limeelezwa kuwa
shida imetokea katika ufafanuzi wa njia itakayotumika kuwalipa
wachezaji hao pesa hizo za ziada.
Wachezaji hao wanaamini kuwa watapokea dola
10,000 kwa ushindi wao wa 1-0 dhidi ya Bosnia-Hercegovina na dola 5,000
kwa sare yao dhidi ya Iran.
Wachezaji hao pia wanadhania kuwa wanapaswa kulipwa dola 30,000 kwa kufuzu katika kundi hiyo.
Hata hivyo, inaaminika kuwa ahadi hiyo ya
shirikisho la soka la Nigeria kwa wachezaji wake ilijumuisha malipo ya
ushindi na kutoka sare na pia asilimia 30 ya pesa watakazolipwa na Fifa
kwa kufika katika raundi ya muondowano.
Inaaminika kuwa kitita hicho kinatarajiwa
kupanda hadi asilimia 40 kama fedha watakazolipwa na Fifa ikiwa Nigeria
watashinda mchuano wao wa raundi ya muondowano, aslimia 50 kwa ushindi
wa robo fainali, asilimia 60 kwa ushindi katika nusu fainali na asilimia
70 kwa kushinda kombe hilo la dunia.
Huku Wahusika wote wakifanya juhudi za kupata
suluhu ya mtafaruko huo , mkufunzi, Stephen Keshi anasisitiza kuwa swala
hilo halitakuwa na madhara yoyote katika timu hiyo.
BBC pia imethibitishiwa kuwa wachezaji hao
watasafiri kwenda Brasilia siku ya Ijumaa kama ilivyoratibiwa na kufanya
mazoezi yao jioni itakayofuata.
Si mara ya kwanza timu ya Super Eagles kuchukua
msimamo kama huo kuhusu fedha. Mwaka uliopita walichelewa kufika katika
michuano ya kombe la mashirika huko Brazil.
No comments:
Post a Comment