Baada ya kukashifu vijana wake kwa kulegeza kamba kwenye Ligi ya
Mabingwa, kocha wa Paris Saint-Germain, Laurent Blanc anatazamia ubora
zaidi wakati watakapoalika Nice katika uwanja wa Parc des Princes
Jumamosi.
PSG walikosa nafasi ya kufuzu raundi ya muondoano baada ya kutoka
sare 1-1 na Anderlecht Jumanne lakini matokeo hayo yalihifadhi hadhi yao
ya kutoshindwa musimu huu katika mashindano yote.
Sasa, wanadhamiria kuongeza mwanya kati yao na wapinzani wa karibu
Lille na Monaco katika kilele cha Ligi Kuu ya Ufaransa, Ligue 1.
Mwaka unakaribia tangu klabu hicho kuchakazwa nyumbani na wana zana
za kuwafurusha Nice waliomo nafasi za kati katika jadwali ambao
wamepoteza mechi tatu kati ya nne za mwisho.
Blanc anatarajiwa kumkaribisha tena Edinson Cavani ambaye amezamisha
mabao tisa kwenye ligi baada ya kukosa mvutano dhidi ya Anderlecht huku
nahodha Thiago Silva pia akishiriki baada ya kurejea baada ya mwezi
mmoja katika sare hiyo.
“Nilitaka ashiriki lakini kwa mpangilio tofauti na ikiwa tulitaka
acheze dhidi ya Nice, ni lazima angepishwa katika mechi ya Anderlecht,”
Blanc alielezea kuhusu kinara wake uwanjani.
Nice wana matatizo langoni huku David Ospina, anayechezea kikosi cha
taifa cha Colombia, akikosa mchezo kwa wiki sita na jeraha la goti huku
kiungo wake wa ziada, Mouez Hassen akibakia nje pia.
Hayo yamefanya chipukizi Luca Veronese, 22, kutumika kama kipa kwa mara ya kwanza Ligue 1.
Monaco wanatazama kukausha machozi ya kushindwa 2-0 ugenini Lille,
mara yao ya kwanza kuonja kichapo, watakapoalika Evian katika uga wa
Stade Louis II Ijumaa.
No comments:
Post a Comment