KWA MAWASILIANO ZAIDI TUMIA BARUA PEPE rockersports212@yahoo.com AU TUPIGIE KUPITIA NAMBARI 0767166607 AU 0717166607. KARIBU SANA. 66666666607 AU 0717166607

Wednesday, November 28, 2012

RAIS TENGA ANASEMA MISHAHARA YA MAKOCHA WA KIGENI NI AHADI YA RAIS KIKWETE HIVYO LITAKWISHA KWA MAZUNGUMZO.

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzaniua (TFF) Leodegar Tenga amesema kuwa shirikisho lake lina imani kuwa mazungumzo baina yake na Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na michezo pamoja na Mamlaka ya Mapato yatamaliza tatizo la kushikiliwa kwa akaunti ya Shirikisho kutokana na malipo ya kodi ya mishahara ya makocha wa kigeni.
Rais Tenga alikuwa akizungumza na waandishi wa habari juu ya uamuzi wa TRA kushikilia akaunti ya TFF ikiielekeza Benki ya NMB kukata kiasi cha Sh 157,407,968/- ikiwa ni malipo ya Kodi Kadri ya Mapato ya Mfanyakazi  (P.A.Y.E) ya makocha Marcio Maximo na wasaidizi wake.
Katika mzozo huo wa muda mrefu, TFF imekuwa ikijitetea kuwa haiwezi kulipa kodi hiyo kwa kuwa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo ndiyo mlipaji wa mishahara ya makocha hao, ikiwa ni ahadi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano, Dk Jakaya Kikwete ya kulipia makocha wa michezo tofauti, ukiwemo mpira wa miguu.
“Hili ni suala nyeti ambalo linahitaji kumalizwa kwa mazungumzo baina ya pande zote,” alisema Tenga na kuongeza: “Ninataka kuwahakikishia kuwa suala hili linazungumzwa na tayari nimeshafanya mazungumzo na maofisa wa Wizara na tumekubaliana kukutana na pande zote  wakati wowote  iwe leo jioni au kesho.
“Ni matumaini yangu kuwa suala hili litakwisha na jana nimetoka Kampala (Uganda kwenye Kombe la Chalenji) moja kwa moja na kwenda kuzungumza na viongozi wa Wizara na wamekubali kwamba tuongee pande zote kulimaliza suala hili.
“Nimezungumza na wenzetu wa serikali kwa sababu najua unyeti wa suala hili. Pesa zilizokamatwa si zetu; ni pesa za klabu na zimetolewa na mdhamini ambaye tumakubaliana namna ya kuzitumia. Fedha hizi hazikutolewa kwa ajili ya kulipia kodi. Lakini TRA wanazishikilia kwa sababu Premier League iko chini ya TFF.”
Tenga alisema kuwa TRA wanafanya kazi kwa kufuata sheria zao za ukataji kodi na hivyo wana haki ya kufuatilia kwa kuwa kwa mujibu wa sheria, muajiri ndiye anayetakiwa kukata kodi kutoka kwenye mshahara wa mfanyakazi.
“Hivyo hatuwezi kuilaumu TRA kwa sababu ndivyo sheria inavyosema, lakini pia hatuna uwezo huo wa kulipa fedha hizo kwa sababu, kwanza hatuna na pili sio sisi tunaolipa mishahara ya hawa makocha,” alisema Tenga.
Akizungumzia historia ya suala hilo, Tenga aliishukuru serikali kwa msaada ambao imekuwa ikiutoa katika mpira na kwamba ahadi ya Rais Kikwete ya kusaidia kulipa makocha wa timu za taifa imeusogeza mpira wa miguu karibu na serikali na karibu na rais.
“Rais Kikwete alisema wakati alipoingia madarakani (mwaka 2005) kuwa anajua kuwa kuna tatizo kwenye mpira na akatoa ahadi ya kulipa walimu wa mpira. Ahadi hiyo imefanya ukaribu uliopo sasa kati ya mpira na serikali; kati ya mpira na rais sasa kuwa mkubwa. Serikali imechangia kwa kiasi kikubwa kwenye mpira, yaani kulipa walimu,” alisema Tenga.
“Sasa sisi ni administrators wa hawa walimu. Tunachofanya ni kuandaa mikataba ambayo ni standard duniani kote kwa mujibu wa taratibu za FIFA (Shirikisho la Kimataifa la Vyama vya Mpira wa Miguu). Kwa kawaida makocha wa kigeni huwa wanatayarishiwa mikataba ambayo ni tax free (isiyo na kodi). Baada ya kuingia nao mikataba, huwa tunaipeleka wizarani ambao ndio wanawalipa makocha moja kwa moja kwenye akaunti zao.”
Katika mkutano huo na waandishi, Rais Tenga pia aliipongeza timu ya taifa ya Tanzania Bara, Kilimanjaro Stars kwa kuanza vizuri mashindano ya Kombe la Chalenji, akisema ushindi huo ni ishara nzuri hasa kutokana na ukweli kuwa kikosi hicho kinaundwa na wachezaji wengi chipukizi na akataka Watanzania waendelee kuiunga mkono.
Tenga pia alisema kumekuwepo na malalamiko kuhusu makato ya mechi na kwamba suala hilo ni la muda mrefu na kwamba TFF imepiga hatua kubwa tangu ilipoanza kulishughulikia.

No comments:

Post a Comment